Contribute to the Physical, Mental and Spiritual Development of the Tanzania people through facilitating the Provision of Quality Social Services to all the people regardless of Colour, Race and Creed

Wednesday, September 18, 2013

UKEREWE LAB INAUGURATION- CSSC SPEECH


TAARIFA YA MKURUGENZI WA TUME YA KIKRISTU YA HUDUMA ZA JAMII (CSSC) KWA MHE. RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA DK. JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA UZINDUZI WA JENGO LA MAABARA YA HOSPITAL YA WILAYA YA UKEREWE-TAREHE 7-SEPTEMBA-2013

MHE RAIS:

 Tume ya kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC) kupitia mradi wake wa ART inaratibu huduma za kupunguza maambukizi toka kwa mama kwenda kwa mtoto na pia huduma za tiba kwa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (yaani WAVIU) katika wilaya zote za mkoa wa Mwanza ikiwemo wilaya ya Ukerewe. Mradi huu unafadhiliwa na watu wa Marekani kupitia taasisi yake ya CDC. Mpaka sasa mradi huu wa ART unaratibu huduma katika vituo vya tiba vipatavyo 69 (9 Ukerewe) na vituo vya kuzuia maambukizi toka kwa mama kwenda kwa mtoto vipatavyo 311 (29 Ukerewe) mkoani Mwanza. CSSC kwa kushirikiana na kamati ya usimamizi wa afya ya mkoa, kamati za usimamizi wa afya za wilaya na wadau wengine, imekuwa inachangia utoaji wa huduma hizi katika maeneo yafuatayo:- Ushauri wa kitaalamu (Technical Assistance), mafunzo kwa watumishi, madawa na vifaa tiba pamoja na rasilimali fedha kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli endelevu za tiba ya Ukimwi.

 
MHE RAIS:

Mbele yako ni jengo la kisasa la maabara utakalolizindua leo lililojengwa kwa ufadhili wa watu wa Marekani kupitia taasisi yake ya Centers for Disease Control and Prevention (CDC) katika mkakati wake wa kuchangia upatikanaji wa huduma bora na salama za maabara nchini. Maabara hii ni mojawapo ya maabara sita za wilaya nchini zilizofaidika na mkakati huu, nyingine ni Bagamoyo (Pwani), Ludewa (Njombe, Siha (Kilimanjaro), Karume (Kilimanjaro) na Micheweni (Pemba).

 
MHE RAIS:

Hadi kukamilika kwa ujenzi huu, wadau mbali mbali walishiriki kwa namna moja ama nyingine katika kuufanikisha ujenzi huu wakiwemo kamati ya Usimamizi wa afya ya mkoa wa Mwanza, kamati ya usimamizi wa afya ya wilaya ya Ukerewe na washirika wenzetu wa AIDSRelief/LEAD waliokuwa wadau wa Ukimwi hapo awali na pamoja na  timu ya maabara ya CDC Tanzania.

 
MHE RAIS:

Matarajio ya CSSC ni kuona maboresho haya ya miundombinu ya maabara hii yanachangia kwa kiasi kikubwa katika ufuatiliaji wa watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi waliojiunga na huduma za tiba wilayani Ukerewe (routine clinical assessment) pamoja na kutoa huduma bora za kiuchunguzi kwa wagonjwa katika hospitali hii ya wilaya. Vile vile kurahisisha kwa kiasi kikubwa ufuatiliaji wakaribu wa watoto na  wakina mama wajawazito wenye maambukizi katika kipindi hiki ambapo mikoa sita ya Tanzania ukiwemo mkoa wa Mwanza inaanza kutekeleza mkakati wa utoaji wa huduma za kuzuia maambukizi toka kwa mama kwenda kwa  mtoto wa Option B plus. Ambapo mama mjamzito mwenye maambukizi ataanzishiwa dawa za kufubaza virusi vya ukimwi-ARV mara moja pindi anapogundulika kuwa na maambukizi, ili kupunguza kiwango cha maambukizi toka asilimia 26 (2011) kwenda asilimia 5 ifikapo mwaka 2015 na kufikia malengo ya kuwa na kizazi salama kisicho na maambukizi nchini.

MHE RAIS:

Mwisho ninaomba kukupongeza wewe binafsi pamoja na serikali za Tanzania na Marekani kwa kazi kubwa iliyofanyika katika  kuboresha huduma  endelevu za tiba hapa nchini. CSSC itaendelea kushirikiana kwa karibu na serikali katika ngazi ya taifa, mkoa na wilaya pamoja na wadau wote wa afya mkoani Mwanza katika kuboresha afya za wanaoishi na virusi vya ukimwi ili waweze kushiriki katika shughuli za maendeleo.

 
MHE RAIS: NAOMBA KUWASILISHA!

 

 

No comments:

Post a Comment